MACHANGU AZIOMBA MAHAKAMA KUONGEZA ADHABU KWA WAHALIFU WA UBAKAJI NA ULAWITI



                                          ALIYEKUWA MBUNGE WA VITI MAALUM MKOA WA KILIMANJARO, KUPITIA CHAMA CHA MAPINDUZI  BETTY MACHANGU

MOSHI.

MAHAKAMA nchini zimeombwa kutoa adhabu kali kwa wanaume ambao wamekuwa wakipatikana na hatia ya ubakaji na ulawi kwa watoto ili kuwa fundisho na kusaidia kupunguza matatizo hayo ambayo yameonekana kushamiri.

Kauli hiyo ilitolewa na aliyekuwa Mbunge wa viti maalum kupitia mkoa wa Kilimanjaro, Betty Machangu (CCM) alipozungumza na waandishi wa habari ambapo alisema kuwa, wanaume wanaofanya vitendo hivyo wamekuwa wakichangia kwa asilimia kubwa kuwaharibia maisha watoto hao.

Machangu alisema kuwa, kutokana na kumuharibia mtoto maisha mwanaume huyo anapaswa kupewa adhabu kali ambayo itakuwa fundisho kwa jamii nzima kutambua kuwa kufanya hivyo ni kosa kinyume na sheria na adhabu yake huwa ni kali.

“Vitendo hivi vimekuwa vikikuwa kwa kasi sana kutokana na mahakama kutoa adhabu ndogo kwa wahusika wanaofanya hivi vitendo hivyo niiombe mahakama iangalie upya adhabu ambazo wamekuwa wakizitoa kwa hawa wahusika na waongeze” alisema Machangu.

Mbunge huyo alitoa mfano hukumu iliyotolewa mwishoni mwa wiki iliyopita katika mahakama ya hakimu mkazi mkoani Tabora, ambapo ilimtia hatiani Sadick Masunzu (47), kwa kosa la kumbaka binti yake mwenye umri wa miaka 16 na kumpatia ujauzito ambapo alihukumiwa kutumikia kifungo cha miaka 4.

Alisema kuwa, adhabu hiyo aliyopewa Masunzu ni ndogo ukilinganisha na kosa alilolifanya ambapo amemuharibia  binti yake maisha kwa kumbebesha mimba.

“Inasikitisha sana kuona mtu ametiwa hatiani kwa kosa la kubaka alafu anahukumiwa kifungo cha miaka minne hii ni aibu sana tunawaomba mahakimu muangalie upya hizi adhabu vinginevyo vitendo hivi vya ubakaji na ulawiti vitaendelea kutokana na adhabu kuwa ya kawaida tu” alisema Machangu.

Aidha Machangu aliiomba jamii kuwa mstari wa mbele katika kuwafichua wanaume ambao wamekuwa wakiwafanyia watoto wa kike unyama huo ili waweze kuchukuliwa hatua stahiki na kukomesha vitendo hivyo.

Mwisho……………….

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Ufahamu ugonjwa wa Ngiri ( Hernia) kiundani zaidi

Mama ajifungua mapacha wenye baba tofauti

UVCCM SIHA YAZINDUA KAMPENI YA KUGAWA TAULO ZA KIKE KATIKA SHULE ZA MSINGI NA SEKONDARI