VIONGOZI WA CHAMA CHA MAPINDUZI NA JUMUIYA ZAKE WATAKIWA KUACHA KULALAMIKA NA BADALA YAKE WASHIRIKIANE KUTATUA KERO ZA WANANCHI…..




MOSHI.

MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama cha Mapinduzi (CCM), mkoani Kilimanjaro Daudi Mrindoko amewataka viongozi wa chama na jumuiya kuanzia ngazi ya kata kuacha tabia ya kulalamika na badala yake wajitoe kuhakikisha wanatafuta ufumbuzi matatizo yanayowakabili Wananchi ili waendelee kukiamini chama.

Mrindoko alitoa kauli hiyo jana wakati wa maadhimisho ya wiki la juma la wazazi wilaya ya Moshi mjini ambapo walipanda miti zaidi ya 200 katika shule ya Sekondari ya Kibo inayomilikiwa na Jumuiya hiyo.
MWENYEKITI WA JUMUIYA YA WAZAZI YA CCM MKOA WA KILIMANJARO, DAUDI MRINDOKO.
Alisema kuwa, wapo baadhi ya viongozi wamekuwa na tabia ya kujenga lawama kwa viongozi wa juu bila kutambua kuwa hata wao wanajukumu la kuhakikisha wanashirikiana kutafuta ufumbuzi wa matatizo yanayowakabili Wananchi.

“Wapo baadhi ya viongozi wamekuwa wakiwabebesha mizigo na lawama viongozi wa juu wakati misingi ya chama chetu ni kushirikiana viongozi wote kuhakikisha tunawatumikia Wananchi na kuwatatulia matatizo yao ili waendelee kukiamini na kukipenda chama chetu” alisema Mrindoko.

Akizungumzia swala la maadili kwa vijana Mwenyekiti huyo alisema kuwa, swala la maadili lipo chini ya Wazazi na kuwataka wanachama wa Jumuiya hiyo kuwa mfano bora katika kusimamia maadili na malezi ili kuwafanya jamii kuiga mfano bora toka jumuiya hiyo.

Aidha Mrindoko alisema kuwa, Jumuiya hiyo ambayo ni kongwe katika mkoa wa Kilimanjaro ilikuwa ikimiliki vitega uchumi mbalimbali zikiwamo shule lakini wapo baadhi ya viongozi wenye uchu binafsi waliuza baadhi ya shule na kudai kuwa katika kipindi chake cha uongozi hatakubali kuona mali za jumuiya zikiuzwa na badala yake atazisimamia kwa ukaribu ili kuona zinanufaisha jumuiya na chama.

Katika hatua nyingine, Mwenyekiti huyo alisema kuwa, zipo baadhi ya shule za Jumuiya ambazo zimefungwa kutokana na kukosa Wanafunzi na kuwataka Wanachama wa ccm pamoja na wawekezaji wanaotaka kuwekeza katika Elimu kufika katika ofisi za Jumuiya ya Wazazi mkoa ili kuona uwezo wa kuendeleza shule hizo zilizofungwa.

Kwa upande wake, Mjumbe wa Baraza kuu la Wazazi Taifa, Alhaji Mollel aliwataka viongozi wa chama na Jumuiya kuimarisha chama kwa kuongeza wanachama ili pindi miaka mitano ya uongozi wao itakapokwisha wajivunie kwa kuacha historia nzuri.

MJUMBE WA BARAZA KUU LA WAZAZI TAIFA, ALHAJI MOLLEL.
Mollel alitumia nafasi hiyo kuwataka viongozi wa dini kuacha kuponda maendeleo yanayofanywa na viongozi wa Serikali na kubaki katika misingi yao ya Biblia na Misaafu, na kuachana na kuhubiri siasa katika Nyumba za ibada.

“Viongozi wa dini mnapaswa kutenga maswala ya dini na kisiasa kwani kila jambo linasehemu yake na mnapaswa kutambua kuwa katika nyumba za Ibada wapo waumini wa vyama mbalimbali hivyo mnaweza kusababisha mpasuko ndani ya nyumba za ibada” alisema Mollel.

Naye Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Moshi mjini, Juma Mohamed alisema kuwa, lengo la Jumuiya hiyo katika wilaya ya Moshi mjini ni kuhakikisha inaboresha Elimu hususani katika shule ya Sekondari ya Kibo ambayo inamilikiwa na Jumuiya hiyo pamoja na kusimamia maadili.

Mohamed alisema kuwa, kipindi cha nyuma Jumuiya hiyo imedharaulika machoni pa watu kwa kushindwa kusimamia maadili na kudai kuwa kwa sasa wamejipanga kurudisha heshima na kudai kuwa hawatamvumilia mtu atakayekuwa chanzo cha kukwamisha malengo yao.

Mwisho…..




































Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Ufahamu ugonjwa wa Ngiri ( Hernia) kiundani zaidi

Mama ajifungua mapacha wenye baba tofauti

UVCCM SIHA YAZINDUA KAMPENI YA KUGAWA TAULO ZA KIKE KATIKA SHULE ZA MSINGI NA SEKONDARI