ZIARA YA MWENYEKITI WA UVCCM MKOA WA KILIMANJARO WILAYANI ROMBO YAIBUA MADUDU…..WATUMISHI WA HALMASHAURI WADAIWA KUFUJA FEDHA ZA VIJANA WENYEWE WASHINDWA KUJITETEA…
ROMBO.
ZIARA
ya Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM), mkoa wa
Kilimanjaro Ivan Moshi, imeibua madudu katika halmashauri ya wilaya Rombo baada
ya kubainika Watumishi wa halmashauri hiyo pamoja na Madiwani wake wamekuwa
wakikopeshana fedha zinazotengwa kwa ajili ya vikundi vya vijana.
Mwenyekiti
huyo aliyefanya ziara hiyo jana na kukutana na Wajumbe wa Baraza kuu la vijana
wilaya, ambapo wajumbe hao waliibua mambo mazito ambayo yamekuwa yakifanywa na
Watumishi wa halmashauri hiyo huku.
Katika
hali ya kushangaza Afisa Maendeleo Vijana
wa Halmashauri hiyo, Florentine Langu
aliyetakiwa kuwepo katika kikao hicho kwa niaba ya Afisa Maendeleo ya Jamii wa
Halmashauri hiyo, ili aweze kujibu tuhuma hizo alifika wakati wanahitimisha
kikao hicho kutokana na kile alichodai kuwa alizuiwa na Kaimu Mkuregenzi wa
Halmashauri ya Rombo, ambaye ni Mhandisi wa Maji aliyetambulika kwa jina moja
la Msangi.
Wajumbe hao wa baraza walisema kuwa, Watumishi
hao wa Halmashauri pamoja na Madiwani wamekuwa wakiunda vikundi vyao binafsi ni
kujikopesha fedha hizo ambazo ni asilimia tano ya mapato ya ndani huku
vikundiambavyo vimekuwa vikiundwa na vijana vikikosa fedha hizo kutokana na
kile wanachoelezwa kuwa hawana sifa ya kukopa.
Afisa Maendeleo huyo wa Vijana,
Florentine Langu alipotakiwa kujibu tuhuma hizo zilizoelezwa na wajumbe wa
Baraza hilo, alishindwa kukanusha au kukubali na badala yake alitoa orodha ya
vikundi 27 ambavyo vimepatiwa mkopo na Halmashauri.
Kutoa kwa orodha hiyo kuliibua kelele
na maswali mengi kutokana na orodha ya vikundi hivyo kuwa ni hewa ambapo
havijulikana huku vikundi vikinge vikitajwa kunufaika na mkopo ili hali
havijapatiwa fedha yoyote.
Hali hiyo ya sintofahamu ilimlazimu
Mwenyekiti wa mkoa kuahidi kulifikisha swala hilo katika ngazi za juu ili
kuhakikisha kuwa Vijana wa Rombo wanapata haki yao ya msingi inayotolewa na
Serikali kwa ajili ya kuwakwamua kiuchumi.
Moshi alisema kuwa, Umoja wa Vijana
mkoa wa Kilimanjaro umejipanga kuhakikisha wanatetea maslahi ya vijana wa mkoa
huo huku akiwataka Viongozi kuhakikisha vijana wananufaika na fursa
zinazotolewa na Serikali.
“Huu ni wakati ambao viongozi
tunapaswa kuacha tabia ya kuongoza kimazoea na badala yake tutafute mbinu za
kuwainua vijana kimaendeleo na kutetea maslahi yao binafsi na pindi unapoona
mtumishi wa Serikali anataka kuchezea maslahi ya vijana usimfumbie macho
mripoti kwetu ili na sisi tumfikishe panapohusika” alisema Moshi.
Kwa upande wake, Katibu wa UVCCM mkoa
wa Kilimanjaro, Abdulrahimu Hamad alisema kuwa, vijana wamekuwa wakitumika
kipindi cha uchaguzi na pindi viongozi wanapopatika wamekuwa wakiwasahau na
kuwataka vijana kutokubali kufanywa tambara la dekio.
Hamad alisema kuwa, viongozi wote bila
kujali itikadi ya vyama wanawajibu wa kuyasimamia maendeleo ya vijana na sio
kuwatumia kwa maslahi yao binafsi.
“Vijana tumekuwa tukitumika kufanya
maandamano na kuvuruga amani ya nchi yetu wakati katika maandamano hayo pindi
mnapata matatizo viongozi hao wanaowaeleza muandamane wamekuwa hawawasaidii kwa
chochote ifike mahali na sisi tusikubali kutumika ovyo kwa maslahi ya mtu
mwingine” alisema.
Mwisho…………..
Maoni
Chapisha Maoni